WENGER AELEZEA MAJALIWA YAKE ARSENAL. - Mazengo360

Monday, 4 September 2017

WENGER AELEZEA MAJALIWA YAKE ARSENAL.

MENEJA wa Arsenal Arsene Wenger amesema “alisita” kusaini mkataba mpya msimu uliopita akiwa na mashaka iwapo kama bado “ana uwezo wa kuongoza klabu hiyo”.

Wenger
Kocha wa Arsenal Arsene Wenger akiwa na wenzake katika benchi la Ufundi.

Wenger alikubali kusaini mkataba wa miaka miwili mwezi Mei, mwezi mmoja tu kabla ya mkataba wake kumalizika.

Akizungumza na kituo cha televisheni cha Ufaransa, katika kipindi cha michezo cha Telefoot, alisema kulikuwa na “sababu binafsi” zilizomfanya kuchelewa kusaini mkataba mpya katika klabu hiyo ambayo ameiongoza kwa miaka 21.

Lakini aliongeza kusema: “Nimekuwepo pale kwa muda mrefu, na najiuliza kama naweza kuipeleka timu katika ngazi nyingine?”

Arsenal walimaliza katika nafasi ya tano katika ligi kuu msimu uliopita- ikiwa ni mara ya kwanza kumaliza nje ya nne bora tangu Wenger alipojiunga na Arsenal mwaka 1996. Hata hivyo Arsenal walishinda Kombe la FA kwa kuwafunga Chelsea.

“Nimekuwepo Arsenal kwa miaka mingi na msimu uliopita tulisumbuka sana,” amesema Mfaransa huyo, 67.

“Mwaka huu tulishinda mchezo wetu wa kwanza, hatukuwa vizuri kwenye mechi ya pili, halafu tukaonesha kiwango kibovu.
“Lakini sasa tunahitaji kuibuka tena, na kama kawaida, wakati wa matatizo unahitaji kushinda mchezo ujao.”

Wenger aliulizwa kuhusu dau la Thomas Lemar, 21, wa Monaco katika siku ya mwisho ya dirisha la usajili.

Ada ya uhamisho ya pauni milioni 90 iliripotiwa kuafikiwa lakini Wenger alisema mchezaji huyo “aliamua kubakia Monaco”.

Alipoulizwa iwapo anapanga kurejea tena Monaco kumsajili mchezaji huyo wa kimataifa wa Ufaransa, Wenger alisema: “Ndio. Nadhani ni mchezaji wa kiwango cha juu.”

Pia alisema alitaka kumsajili Kylian Mbappe, ambaye amejiunga na Paris Saint-Germain kwa mkopo na ambao hatimaye utakuwa uhamisho wa pauni milioni 165.7(euro milioni 180) msimu ujao.

“Milioni 180 ni kiasi kikubwa kidogo kwetu,” alisema Wenger, ambaye amemuelezea Mbappe, 18, kama “Pele anayechipukia”.

(Taarifa na picha kwa hisani ya BBC).

MWISHO.