JAMII VIJIJINI IACHENI KUKANDAMIZA WANAWAKE. - Mazengo360

Monday, 17 July 2017

JAMII VIJIJINI IACHENI KUKANDAMIZA WANAWAKE.

JAMII maeneo ya vijijini bado inaendelea na mfumo dume wa kukandamiza wanawake kijinsia na hata kuwanyima haki ya kufaidi matunda ya kazi za kilimo na ufugaji na pia kunyimwa haki ya kumiliki ardhi kijamii kama walivyo wanaume.

Action+Aid+2
Wanawake kijiji  cha Mloda (W) Chamwino, Dodoma.

Hivi karibuni wilayani Chamwino, mkoa wa Dodoma katika kijiji cha Mloda, Kata ya Mlowa Barabarani kulifanyika kongamano la wanawake wanaojishughulisha na kilimo vijijini ambapo walipaaza sauti zao kudai haki sawa kati ya wanawake na wanaume katika jamii.
Kongamano hilo lililofadhiliwa na shirika la Action Aid hapa Tanzania, kupitia mradi wao wa kuwezesha umma kifedha katika sekta ya kilimo, mratibu wa mradi huo Joram Wimmo aliishauri jamii kuhakikisha wanawake wanapatiwa haki kutumia fursa ili kupiga vita umaskini nchini.
Mratibu huyo alieleza bayana kwamba, pamoja na sheria nyingi nzuri zinazolenga kumtetea na kulinda haki za mgawanyo wa mali katika ngazi ya vijiji na kutaja sheria ya mamlaka ya vijiji ya mwaka 1999, kipengele cha tano kinaeleza bayana haki ya jamii kugawana sawa mali za jamii au familia baina ya wanawake na wanaume.
Ni jambo lililo dhahiri kwamba wazalishaji wakubwa vijijini ni wanawake na ndio pia wanao shughulika zaidi katika kilimo ili familia ijipatie chakula cha kutosha na kujiwekea akiba kwa matumizi ya baade.
Pia wanawake ndio wanaotunza na kuangalia watoto katika familia ikiwamo afya zao pamoja na kuhakikisha watoto wanahudhuria shuleni pamoja na kuwakilisha katika vikao namikutano ya wazazi vya shule kuhusu maendeleo ya watoto katika familia.

Action+Aid+3
Wakina mama wakiwasilisha ujumbe wao kwa jamii.

Yapo malalamiko mengi yanayotolewa na akina mama wanoaishi maeneo ya vijijini juu ya ukandamizaji kijinsia, ambapo baada ya kuzalisha mali toka mashambani, akina mama hawapewe nafasi ya kupanga namna ya kutumia matunda ya nguvu zao.
Mkaazi mmoja wa kijiji cha Mloda, Kata hiyo ya Mlowa Barabarani Bi Mariam Chiseo, mwenye umri miaka 53 ameeleza kwa uchungu tabia za wanaume katika kijijini hicho wanavyo kandamiza haki za akina mama na hata kutowaruhusu kufaidi matunda ya kazi zao.
Alieleza manyanyaso hayo yakiwamo haki ya kutoshirikishwa katika kupanga matumizi ya mazao yanayovunwa shambani mfano alizeti, mtama na hata mahindi pamoja na mifugo.
Aliendelea kueleza kwamba, wanawake baada ya kuvuna na kuweka ghalani mazao hayo, baadae hushtukia mme ameshaafikiana na wananunuzi au madalali wa ununuzi na kasha huja kuchukua mazao hayo bilamakubaliano na mkwe na malipo husika hayawasilishwi kwa dhamira ya manufaa ya familia.
Bi Mariam aliendelea kueleza adha wanazozipata wanawake baada ya kuhoji, hupatiwa kipigo na kufukuzwa nyumbani na waumme zao kisha hupotelea maeneo ya minadani kutumia fedha hizo na marafiki pamoja na wanawake wa mitaani.
Ameiomba jamii pamoja na mamlaka zinazohusika kusaidia kutatua tatizo hili kwani limeota mizizi na kuongeza, “kamwe jamii haiwezi kutoka katika umaskini endapo hakutakua na hatua za makusudi za kumkomboa mwanamke kutoka katika ukandamizaji huu” alieleza kwa uchungu.

Bi+Janet+Nyamayahasi
Bi Janet Nyamayahasi.

Nae mwenyekiti wa Jukwaa la wanawake hao Bi Janet Nyamayahasi ambae pia alishapata fursa ya kuwakilisha umoja wa wanawake hao wanaojishughulisha na kilimo maeneo ya vijijini katika vikao vya Umoja wa Afrika nchini Ethiopia, na pia kwenye Baraza la Umoja wa Mataifa (UN) mjini New York Marekani, amesema yeye na wanawake wote wamedhamiria kudai haki yao katika jamii.

Bi Janet aliendelea kutaja malengo ya umoja huo ulioanzishwa mwakajana mwezi Octoba kwa kupanda milima ya Uluguru na Kilmanjaro kupaaza sauti zao ilikupatiwa hakia ameeleza kunyimwa haki ya kumilikishwa ardhi inayomilikiwa kimila na jamii ni kitovu cha kumkandamiza mwanamke na kuchangiaumaskini.
Ameeleza lengo lao kuu ni kuhakikisha wanapatiwa haki ya kumiliki ardhi pindi ifikapo mwaka 2025 na kuomba msaada wa viongozi mbalimbali katika jamii wakiwamo wa mitaa, kiserikali na wa kidini kusaidia kuelimisha umma ili wafikie lengo hilo.
Ametaja masahibu wanawake wanayokutana nayo katika kunyimwa haki hiyo ikiwamo kumfanya mwanamke kama bidha wakati wa kupanga mahari wanapoolewa.
“Wazee wa kimila hukaa katika vikao vyao wenyewe na kukubaliana kiasi cha mahari kitakachobadilishwa na mwanamke, na mara nyingi hua ni mifugo pamoja na fedha zinazopatikana baada ya kupoka sehemu ya mazao yaliyozalishwa na mwanamke katika familia.”
Alifafanua Bi Janet Nyamayahasi kwamba, Jambo hili lina athari kubwa na pia linachangia sana umaskini katika jamii.
Mfano mwingine uliotolewa na Bi Janet ni kuhusu ndoa za utotoni ambapo katika maeneo ya vijijini hususani wilayani Chamwino mkoani Dodoma mtindo huu umeshamiri sana.
Aliendelea kueleza namna wanafunzi wa jinsi ya kike wanapomaliza masomo ya shule za msingi na kukosa nafasi ya kuendelea na masomo ya sekondari, wanavyoingia katika ndoa za utotoni kwa tamaa tuu za wazazi wa kiume kupata mali kwa kubadilishana na motto wa kike.
Amesema “mabinti wengi walio chini ya umri wa miaka 18, wameozwa kwa waume japo sheria inawaruhusu tena kwa waume wenye umri mkubwa na baade kuzalishwa watoto kwa tama tuu za mali, ambapo ni kutanua umaskini katika jamii”, alisema kwa uchungu.
Tatizo jingine linalowakandamiza wanawake na kusababisha jamii ibakie katika umaskini ni unyanyasaji wa kingono ambapo wanawake wa rika zote wakiwamo wenye umri mkubwa hubakwa na wenye fedha mfano wachuuzi wa mifugo na pia wafugaji.
Mabinti wa shule za msingi na sekondari hudanganywa na makundi haya na kufanya vitendo vya ngono na baadae kupata mimba na kufukuzwa mashuleni, kutokana tuu na umasikini unaowakabili katika jamii.
Mwanamke mmoja (jina limehifadhiwa) alitoa malalamiko yake mbele ya umati wa watu katika kongamano hilo kwamba mnao mwaka jana alibakwa na mwanaume mmoja na ushahidi ukaonekana lakini kutokana na nguvu ya fedha na ukandamiza wa mfumo dume, mashtaka yaliyowasilshwa polisi yalibadilishwa toka ubakaji hadi shambulio la kawaida lakimwili, hivyo sheria ikamtia hatiamlalamikiwa na kumtoza faini ya shilingi laki tatu au kifungo miezi sita.
Ushuhuda mwingine wa ukandamizaji ulitolewa na mkazi wa Kata ya Iringa Mvumi, wilayani Chamwino Bi Sona Vumi ambae ni mjane, alisema aliolewa mwaka 1978 na mmewe kihalali na baade mmewe aliugua na mwaka 2010 akafariki dunia.
Dada yake marehemu mmewe (hakumtaja jina) alidiriki kumfukuza katika nyumba na shamba alilokuwa akimiliki yeye na marehemu mmewe na kudai kwamba, hakuja katika familia yao na mali.
Baade Bi Sona Vumi alitoa taarifa katika baraza la Ardhi la Kata na akashinda shauri hilo na kuamuriwa apatiwe haki na mali za marehemu mmewe, lakini mlalamikaji ambae ni wifi yake alienda kukata rufaa katika mahakama ya wilaya kudai kwamba haki ya familia yao inanyang’anya na mwanamke huyo.

Mhe+Salama+Msigwa.
Diwani Mhe Salama Msigwa.

Ili kuhakikisha haki za akina mama zinatetewa, Diwani wa viti maalum (CCM) katika Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Chamwino Mhe Salama Msingwa amewataka akina mama wote wanaonyanyaswa kijinsia, ikiwamo kubakwa na kudhulumiwa haki zao wafikishe malalamiko yao kwenye baraza hilo ili wawasaidie.
Mhe Msigwa alifafanua kwamba, endapo wanawake watabakia kuwa waoga kuchukua hatua dhidi ya unyanyasaji, kwa kuhofia  kutengwa na jamii, wataendelea kunyanyasika na vyombo vilivyopo mfano Baraza la Madiwani kushindwa kuwatetea
Ameeleza pia kwamba, ameshangazwa na shuhuda za manyanyazo zilizotolewa katika kongamano hilo na kusema, hazijafikishwa  kwenye ngazi rasmi za ufuatiliaji na utetezi hivyo, ametoa wito kwa wanawake wote kutoa taarifa pindi wanapokutana na masahibu ya namna hiyo.
Kwa kuhitimisha makala hii ni kwamba, wanawake ndio muhimili mkubwa wa uzalisha mali katika familia mijini na vijijini.
Pia wanawake wanao mchango mkubwa sana kubadilisha hali ya umaskini katika jamii endapo watapewa fursa na hadhi sawa ya kupanga na kutumia mali zinazo zalishwa katika familia.
Vita vya kupambana na umaskini hapa nchini itakuwa rahisi zaidi kama mwanamke watakombolewa katika ukandamizaji na kupatiwa nafasi ya kumiliki mali ikiwamo ardhi kadiri sheria inavyoelekeza, kwani ni waaminifu na wenye kujali zaidi ustawi wa familia.
MWISHO.