MUOMBEENI RAIS JOHN MAGUFULI - Mazengo360

Saturday, 8 July 2017

MUOMBEENI RAIS JOHN MAGUFULI


KANISA Katoliki limewaomba watanzania kumwombea Rais Dkt  John Pombe  Magufuli ili atimize dhamira yake ya kuwapigania wanyonge na kuondoa umaskini nchini kwani kazi hiyo ni ngumu na yenye vikwazo vingi.
Wito huo umetolewa leo mjini Dodoma na Askofu Mkuu wa Jimbo Katoliki la Dodoma Mhashamu Beatus Kinyaia wakati wa mahubiri yake kwenye Ibada maalumu ya Misa ya kutoa daraja la Upadrisho iliyofanyika katika kanisa kuu la Jimbo la Mt Paulo wa Msalaba.
Askofu Mkuu Kinyaia alimwagia sifa Rais Dkt John Magufuli kwa utendaji wake kazi mzuri na mahiri hususani kwa kutetea haki za wanyonge wa Taifa hili na kueleza kwamba, anafurahishwa sana na utendaji wake.
Alisema, “ninawaomba waumini wote na watanzania kwa ujumla kumwombea kwa Mungu Rais Dkt John Magufuli ili aweze kutekeleza azma yake njema ya kuwatetea wanyonge na pia Mungu amwepushe na maadui wabaya,”alifafanua Askofu Kinyaia.

PX+3
Askofu Mkuu wa Jimbo Katoliki la Dodoma Mhashamu Beatus Kinyaia akiwa katika picha ya pamoja na Padre Erasmus Kamugisha  wa Shirika la Kitume la Mapadre wa Mateso ya Yesu (kulia kwake) pamoja na Mkuu wa Shirika hilo hapa nchini Padre Greogory Olomy (kushoto) pamoja na walezi wa padre mpya muda mfupi baada ya kupatiwa daraja la upadre katika kanisa kuu la Mt Paulo wa Msalaba hapo July 07, 2017 mjini Dodoma.

Katika Ibada hiyo ambapo Askofu Kinyaia alitoa daraja la Ushemasi na Upadre kwa watawa wawili hivi leo, aliwataka pia vijana waache kukaa vijiweni na badala yake wafanye kazi kwa bidii na kutumia muda wa ujana wao vizuri ili wajipatie maendeleo na waepuke uvivu.
Akitoa mfano wa utendaji wa Rais Dkt Magufuli, Askofu Kinyaia amewataka vijana kubadilika na kumuunga mkono Rais katika jitihada zake za kuhimiza maendeleo na kuongeza kwamba, hakuna mafanikio yanayokuja kwa maneno matupu hivyo wasikie na kumuunga mkono Rais Magufuli.
Pia amewahusia wafuasi wa kanisa hilo hapa nchini kutekeleza wito wa kufanya kazi kila mtu kwa bidii na ubunifu mkubwa kwani ndio mpango wa mungu kwa wanadamu, na pia ndicho Rais anachohimiza, alieleza Askofu Kinyaia.
Amwahusia watendaji katika kada za ualimu na afya kwamba, kazi zao zinahitaji zaidi wito hivyo waombe kwa mungu awajalie karama ya upendo, uvumilivu na moyo wa kuwasaidia wengine ili wanyonge wapate faraja wanapohitaji huduma zao.
Nae Mkuu wa Shirika la Mapadre wa Mateso ya Yesu hapa nchini Padre Greogory Olomy amemshukuru Askofu Mkuu Beatus Kinyaia kwa moyo wake wa upendo na matashi mema kwa watu wote wa taifa hili, na kuahidi kuendelea kushirikiana nae pamoja na jamii kwa ujumla kuhimiza mambo mema, ili jamii ipate amani.
Pia Mkuu huyo wa Shirika ametoa wito kwa padre na shemasi  ambapo wote wapochini ya shirika hilo kwamba waende kuwasaidia vijana katika jamii kufuata mifano mema kwa kufanya kazi ili wabadilike.
Askofu Mkuu Kinyaia ametoa daraja la Ushemasi kwa Frateri Stephano Omondi ambae ni raia tokea nchini Kenya na pia daraja la Upadrisho kwa Padre mpya Erastus Kamugisha wote wa Shirika la Kitume la Mateso ya Yesu hivi leo mjini Dodoma.

MWISHO.